Tuesday 9 October 2012

MAMBO SIO SHWARI KATI YA KHADIJA KOPA NA MZEE YUSSUF...

Malkia wa Mipasho Bi. Khadija Kopa
Big Daddy A.K.A Mfalme Mzee Yussuf

Imebainika wazi kuwa mambo sio shwari kati ya Malkia wa Mipasho Bi. Khadija Kopa na Big Daddy Mfalme Mzee Yussuf katika ulimwengu wa taarab.

Akithibitisha hayo katika ziara yake hapa mjini Mombasa, Bi. Khadija alisema binafsi ameshangazwa na kukerwa zaidi na kundi la Jahazi kutokana na vitendo wanavyomfanyia.

Alisema baadhi ya waimbaji na viongozi wa kundi hilo wamejenga chuki za wazi wazi dhidi yake, bila sababu yoyote, hali inayompa wakati mgumu.

Khadija alisema mara kadhaa anapoalikwa kufanya maonyesho kwa kushirikiana na kundi hilo, viongozi na wasanii wake humfanyia vituko vya kila aina, ambavyo humfanya wakati mwingine ashindwe kuimba.

"Mara kwa mara ninapoalikwa kuimba pamoja na Jahazi, huwa sipewi ushirikiano. Hunifanyia vituko vingi sana,”alisema.

Mkongwe huyo wa mipasho alisema binafsi hana bifu na uongozi ama msanii yeyote wa kundi hilo na kwamba anawaheshimu.
Pia Khadija alidokeza kuwa , kutokana na vituko anavyofanyiwa na uongozi wa kundi hilo, analiona kama vile limeamua kumdhalilisha na kumvunjia heshima.

Akitoa mfano alisema, katika tamasha la Mitikisiko ya Pwani lililofanyika mwishoni mwa mwaka jana katika ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam, huko Tanzania alilazimika kuimba kwa tabu baada ya Jahazi kuondoa stejini baadhi vyombo vyao.

Kwa mujibu wa Khadija, kuna siku alikodiwa na mfanyabiashara Abbas Shentemba kuimba akiwa na waimbaji wengine pamoja na kundi la Jahazi, lakini alishindwa kufanya hivyo kutokana na kuwekewa ngumu na viongozi wa kundi hilo.

"Nakumbuka nilialikwa pamoja waimbaji wengi, akiwemo Mohamed Iliyas na Afua Suleiman, lakini sikuweza kuimba kutokana na kubaniwa na uongozi wa Jahazi na kila nilipokuwa namkumbusha msimamizi wa onyesho hilo, alinijibu kwa kejeli,”alisema.

"Alianza kupanda jukwaani Afua, wakati anapanda Mohamed Iliyas, nilimtuma mpiga kinanda mmoja wa Jahazi akamwambie yule msimamizi kwamba akiteremka Iliyas nipande mimi, lakini wakampa majibu ya kebehi,”aliongeza.

Akisimulia zaidi mkasa huo, nguli huyo wa mipasho alisema, siku hiyo alipata taarifa mapema kwamba hawezi kuimba na alimfuata aliyemkodi na kumuuliza, lakini alimpa majibu kwamba lazima aimbe.

Alisema baada ya Iliyas kuteremka stejini, alipanda Mzee Yusuf na kuanza kuimba na hapo ndipo alipoamini maneno aliyoambiwa mapema kwamba hawezi kuimba siku hiyo.

“Baada ya Mzee Yusuf kupanda stejini, nilimfuata aliyenialika na kumuaga na yeye akakubali, kwa maana hiyo niliondoka bila kuimba,”alisema Khadija.

"Mimi binafsi ni mtu wa watu, kwa hiyo naomba kama Jahazi nimewakosea kitu, wanambie ili niwaombe radhi na mimi kama wamenikosea waniombe radhi,”aliongeza.
 
"Namheshimu kila mtu, sijawahi kugombana na yeyote, naona Jahazi wanajisumbua kwa sababu kwangu ni watoto wadogo sana," alisema.

Additional information Via RUSHA ROHO Blog...

No comments:

Post a Comment